25 September 2012

Katika kusimamia uongozi unaozingatia misingi muhimu ya haki za binadamu, sheria na utawala bora, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesisitiza msimamo wake wa kutotoa ushirikiano kwa kamati iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Emmanuel Nchimbi kuchunguza kifo cha Mwandishi wa Habari wa Channel ten, Daudi Mwangosi, kilichotokea Septemba 2, 2012, Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa.

Msisitizo huo umekuja baada ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo kukiandikia barua (isiyokuwa na Kumbukumbu Namba) CHADEMA, akiomba kamati yake ikutane na viongozi wa chama Septemba 25, ili kutafakari tukio hilo na matukio ya aina hiyo yaliyowahi kutokea hapa nchini.

Itakumbukwa kuwa Marehemu Mwangosi aliuwawa na Jeshi la Polisi akiwajibika kwa jamii katika shughuli za uandishi wa habari, wakati askari wa jeshi hilo walipovamia ofisi za CHADEMA Kata ya Nyololo na kuanzisha vurugu wakati wanachama walipokuwa wakiendelea na shughuli halali za ndani za chama. Katika barua kwenda kwa Mwenyekiti wa Kamati hiyo, CHADEMA kimesema wazi kuwa hakiko tayari kukaa na kutafakari juu ya kifo cha Mwangosi kama ilivyopendekezwa na kamati hiyo, kwani imeundwa kinyume cha sheria, huku pia ikiwa imeundwa na mtu ambaye kanuni za msingi za utawala bora, zinamtaka awe amejiuzulu au kufukuzwa kazi, kupisha uchunguzi huru juu ya mauaji hayo yaliyofanywa na jeshi la polisi, linalowajibika kwake kama Waziri wa Mambo ya Ndani.
Kamati hiyo pia inawahusisha polisi ambao katika tukio hilo ni watuhumiwa namba moja.

Mbali ya kusisitiza kuwa haiwezi kutoa ushirikiano kwa kamati ambayo haipo kwa mujibu wa sheria, CHADEMA kimeshangazwa na kusudio hilo la Kamati ya Nchimbi kutoa mwaliko wa kutaka kukutana na viongozi wa CHADEMA, huku ikitambua wazi msimamo wa chama hiki juu ya uwepo wa kamati hiyo mara tu ilipoundwa.

Kutoa ushirikiano kwa kamati ambayo haina mamlaka ya kisheria ya kuhakikisha ukweli mtupu unajulikana na haki ionekane ikitendeka kutokana na kifo hicho na vingine vingi ambavyo vimefanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya raia wasiokuwa na hatia, kwa masuala mbalimbali yakiwemo ya kisiasa, ni kuhalalisha uvunjivu wa haki za binadamu, Katiba na sheria za nchi. CHADEMA haiko tayari kuona hali hiyo ikifanyika.
Katika kuonesha msisitizo wa kutokubali mwaliko wa Kamati ya Nchimbi inayotaka kutafakari matukio ya vifo ambapo Jeshi la Polisi limewanyang’anya watu wasio na hatia haki ya kuishi, katika barua yake ya majibu, CHADEMA pia kimeambatanisha nakala ya barua ya tarehe 10/09/2012 iliyowasilishwa kwa Rais, ili kamati hiyo iweze kuelewa msimamo mpana wa chama kuhusu mauaji ya kisiasa yanayofanyika nchini. Kwa taarifa hii, CHADEMA kinaendelea kusisitiza maazimio ya Kamati Kuu ya Chama, ambayo pamoja na mambo mengine, iliazimia kuwa kutokana na mfululizo wa matukio ya mauaji ya kisiasa yanayofanywa na Jeshi la Polisi katika shughuli halali za chama, Waziri wa Mambo ya Ndani Emmanuel Nchimbi, Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Said Mwema, Mkuu wa Operesheni wa Jeshi la Polisi Paul Chagonja na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile wawajibike kwa kujiuzulu au Rais awawajibishe kwa kuwafukuza kazi ili wapishe uchunguzi huru na wa haki.

Pia Kamanda wa Polisi Iringa, Michael Kamuhanda, Kamanda wa FFU Mkoa wa Morogoro, na askari wote wanaoonekana kwenye picha wakiwa wamemzunguka Mwangosi muda mfupi kabla hajalipuliwa na kuuwawa, wakamatwe haraka na kushtakiwa mahakamani kwa tuhuma za mauaji ya Mwangosi.
Kinyume na hapo ni kuchezea akili za wapenda haki na uwajibikaji, ikiwa moja ya misingi ya amani Tanzania na dunia nzima kwa ujumla.
CHADEMA inapenda kusisitiza kuwa itatoa ushirikiano kwa chombo kitachoundwa kwa mujibu wa Sheria huku ikitilia msisitizo wito kwa Rais kuunda Tume ya Kimahakama/Kijaji kuchunguza vifo vyote vyenye utata na vinavyohusishwa na masuala ya kisiasa kama tulivyopendekeza kwake hapo kabla.
Imetolewa leo Septemba 24, 2012
Dar es Salaam na; Tumaini Makene
Ofisa Habari wa CHADEMA
chanzo: fredynjeje.blogspot.com  

0 comments:

Post a Comment

.

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!