29 May 2014


Serikali ya Qatar imezindua kampeini ya kuwasihi watalii kuvalia mavazi ya heshima wanapokuwa katika maeneo ya umma na pia kuheshimu maadili ya kiisilamu nchini humo.

Kupitia kwa Twitter na Instagram, serikali hiyo inaweka picha zinzoonyesha ambavyo watalii wanapaswa kuvalia wakiwa nchini humo pamoja na kuonyesha mavazi yasiyoruhisiwa.

Hii ni kampeini ya kupitia kwenye mitandao ya kijamii kwa watu wanaonuia kusafiri kwenda Qatar.

Mavazi kama nguo fupi, zisizo na mikono mirefu na vitopu vifupi, yameharamishwa, wakati wanaume hawaruhusiwi kuvalia kaptula na vesti huku wakionyesha vifua vyao.

Kauli mbiu ya kempeini hiyo ni'' Ukiwa Qatar wewe ni mmoja wetu. Tusaidie kuendeleza maadili na utamaduni wa Qatar , tafadhali valia mavazi ya heshima. ''

Kampeini hiyo inawaomba watu kufunika mabega yao na magoti na kujizuia kuvalia stockings.

Kituo cha utamaduni wa Qatar, kimewahi kuzindua kampeini kama hii ili kuwafunza watalii kuhusu mavazi yao.

"kiwango cha watu kuvalia nguo zisizo za heshima, kimeongezeka hasa katika maeneo ya umma ikiwemo katika maduka makubwa ya kifahari,'' alisema Nasser Al Maliki, afisaa mkuu wa mawasiliano katika kituo hicho.

"hatutaki watoto wetu kuishi katika mazingira kama haya na kuweza kujifunza mambo yasiyokubalika na ndio maana tunafanya kampeini hii. ''

Qatar, ni mwenyeji wa michuano ya kombe la dunia mwaka 2022 na ina takriban watu milioni 2 na pia hutumia sheria ya kiisilamu katika mfumo wake wa sheria.

Raia wa Uingereza 17,500, wanaishi katika nchi hiyo na nchi hiyo pia hupokea wageni 40,000 kila mwaka.

Kuvalia nguo zinazoonekana kukosa heshima ni kinyume na sheria sawa na ilivyo kutoa matamshi ya matusi au kufanya kitendo chochote kisichokubalika katika sehemu ya umma.

Ikiwa atapatikana na hatia mtu anaweza kufungwa jela miezi sita au kutozwa faini.



0 comments:

Post a Comment

.

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!