17 July 2013


Sisi wananchi wa Tanzania: 

Tukiwa ni wapiga kura wa majimbo mbalimbali nchini Tanzania, tumechukua jukumu leo kutoa wito kwa wabunge na serikali kufuta tozo/kodi mpya ya laini za simu iliyoanza kutumika baada ya sheria kupitishwa na Bunge Juni 2013. 
Hii ni sehemu muhimu ya wajibu wetu kama raia waaminifu, wenye nia njema ya kuchangia mawazo bora yatakayotuletea maendeleo endelevu nchini kwetu. 
Bila mjadala mpana na mawazo chanya yaliyochambua masuala kwa undani kama msingi wa maamuzi, nchi itafanya maamuzi dhaifu yasiyosimama kwenye misingi ya hoja na ukweli wa mambo. 
Kukaa kimya kwenye jambo ambalo tunaliona linakandamiza wananchi na huenda likaturudisha nyuma kimaendeleo, ni kushindwa kuwajibika kama wananchi.

Tunapinga kodi ya laini za simu

KWA SABABU:- Sisi wananchi hatujashirikishwa kupitia mjadala wa Bunge kuhusu kodi hii kwani Waziri wa fedha hakusoma hiki kipengele wakati wa hotuba yake na tulikosa taarifa mpaka baada ya kupitishwa kwa sheria ya kodi hii.

KWA SABABU:- Kodi hii inamkandamiza mtanzania wa hali ya kawaida na wa hali ya chini ambao ni 67% ya wananchi wanaoishi chini ya kipato cha dola 1.25 (shs 2,000) kwa siku. Takwimu zinaonyesha kuwa kati wa wamiliki wa laini za simu milioni 22, milioni 8 wanatumia chini ya shilingi 1,000 kwa mwezi. Kuwaongezea mzigo wananchi hawa kwa kiwango ambacho tayari wanashindwa kumudu ni kuwanyima kabisa fursa ya kutumia huduma hii muhimu.

KWA SABABU:- Kodi hii haifuati misingi ya kulipa kwa kadri ya matumizi na ni kodi kandamizi inayowatoza wamiliki wa laini ya simu wote kiasi kimoja bila kuzingatia kiwango cha matumizi. Hii inamkandamiza mwananchi wa hali ya chini kwa kumlazimisha kulipa kiwango kikubwa cha kodi kulingana na mapato yake. Tukichukulia mfano wa mtu anayetumia shilingi laki tano kwa mwezi kama muda wa maongezi na yule anayetumia shilingi elfu tano - na tukilinganisha uwiano wa malipo haya na matumizi yao – basi yule anayetumia shilingi laki tano analipa 0.2% ya matumizi yake, ila yule anayetumia shilingi elfu tano anatozwa 20% ya matumizi yake.

KWA SABABU:- Kodi hii ni juu ya ongezeko la kodi mbalimbali katika huduma za simu za mkononi ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa ushuru kutoka 12% kwenda 14.5% na pia kodi hii kutozwa kwa huduma zote ingawa awali ilitozwa kwa huduma ya matumizi ya kuongea. Hivi sasa utumiaji wa internet, kutuma na kupokea pesa kwa njia ya simu za mkononi unatozwa kodi. Ongezeko hili pekee limeshafanya huduma za simu za mkononi kupanda gharama kwa kiasi kikubwa. Ongezeko hili la shs 1,000 litazidi kuwaumiza wananchi.

KWA SABABU:- Kodi hii pekee inampunguzia mtumiaji muda wa maongezi na huduma zingine za simu za mkononi ikiwa ataendelea na matumizi yake ya mwezi kama kawaida. Kwa mfano mtumiaji akitumia kifurushi cha bei ya shs 475 inayompa dakika 20 za maongezi, 50 MB za data, na sms 100 kwa masaa 24, kwa kodi ya shs 1,000 kwa mwezi ni sawa na serikali kuchukua siku mbili za kifurushi hiki kila mwezi au ni sawa na kuchukua dakika 40 za maongezi, 100MB za data na sms 200 kila mwezi.

KWA SABABU:- Huduma ya simu za mkononi siyo anasa na ni sehemu muhimu ya mawasiliano na kiungo kinachochangia kurahisisha harakati za maendeleo. Kwa mfano wakulima hutumia huduma hizi katika kuuza mazao yao na kupokea fedha; akina mama wajawazito hupelekewa taarifa muhimu kuhusu afya zao; wanafunzi kupitia internet wanaweza kupata habari muhimu zinazohusiana na masomo yao nk. Kodi hii itawanyima fursa ya kutumia huduma hizi muhimu.

KWA SABABU:- Serikali inaweza punguza matumizi yake mengineyo (safari, posho, semina, manunuzi ya magari na kudhibiti ufisadi) hivyo kufidia pengo litakalosababishwa na kusitisha tozo/kodi ya laini ya simu.

KWA SABABU:- Pia, utafiti uliofanywa na Interfaith Standing Committee on Economic Justice and the Integrity of Creation mwaka jana uligundua kuwa kwa wastani Tanzania hupoteza dollar billion moja (takriban shs trilioni 1.8) kila mwaka kutokana na ukwepaji kodi, uhamishaji harama wa fedha na misamaha ya kodi. Tunaitaka Serikali yetu iongeze ufanisi wa kukusanya kodi kutoka vyanzo vilivyopo tayari na kuondoa misamaha kwa hivyo itaziba pengo la shs billioni 264 kutoka kwa kodi ya laini ya simu za mkononi. 

MWISHO
Tunakuomba ufikishe ujumbe kwa wengine kwa kuwapa link ya hii petition ili nao washiriki maamuzi haya muhimu

Source jestina George blog

0 comments:

Post a Comment

.

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!